Kitasa TRA United mlangoni Yanga

Joel JJ By Joel JJ • 6th June 2026


Kitasa TRA United mlangoni Yanga

Mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara kwa misimu minne mfululizo, Young Africans SC, wanatajwa kuonyesha nia ya kumsajili beki wa kati wa TRA United FC, Nassri Kombo, kuelekea dirisha kubwa la usajili la msimu ujao.

Kombo, mwenye umri wa miaka 23, amekuwa miongoni mwa wachezaji waliovutia zaidi msimu huu kutokana na kiwango chake thabiti akiwa na TRA United. Uwezo wake wa kucheza kwa utulivu, kusoma mchezo kwa haraka na uimara wake katika safu ya ulinzi vimemfanya kuwa mmoja wa mabeki wanaofuatiliwa kwa karibu na klabu kadhaa, huku Yanga ikitajwa kuwa mbele katika kinyang’anyiro hicho.

Taarifa zinaeleza kuwa Yanga imepanga kuongeza beki wa kati mzawa katika kikosi chake ili kuendelea kuimarisha ushindani wa ndani ya timu. Hatua hiyo inakuja wakati klabu hiyo ikitafuta mbadala wa Frank Assink, ambaye kwa sasa anaitumikia Yanga kwa mkopo akitokea Singida Black Stars.

Usajili wa Kombo unaweza kuipa Yanga nafasi ya kuendelea kujenga msingi imara wa mabeki wazawa, huku klabu hiyo ikielekeza nguvu zaidi katika kusajili wachezaji wa kigeni kwenye maeneo mengine muhimu, hususan safu ya kiungo na ushambuliaji.

Kwa sasa, Yanga haina presha kubwa katika eneo la ulinzi wa kati kutokana na uwepo wa mabeki wenye uzoefu kama Ibrahim Bacca, Bakari Mwamnyeto na Dickson Job, ambaye anatarajiwa kurejea kikosini wakati wa maandalizi ya msimu mpya (pre-season).

Mkataba wa Kombo na TRA United unatarajiwa kufikia tamati mwishoni mwa msimu huu, jambo linalomfanya kuwa miongoni mwa wachezaji wanaoweza kupatikana kwa urahisi katika soko la usajili.

Iwapo dili hilo litakamilika, Yanga itaongeza nguvu mpya katika safu yake ya ulinzi huku ikiendelea kujijenga kwa ajili ya ushindani wa ndani na michuano ya kimataifa.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.