Klabu ya Real Madrid inaripotiwa kuandaa ofa kubwa ya pauni milioni 130 (zaidi ya Shilingi bilioni 455) kwa mabingwa wa Ujerumani, Bayern Munich, ili kumsajili winga wa kimataifa wa Ufaransa, Michael Olise.
Kwa mujibu wa taarifa za karibu na klabu hiyo, rais wa Real Madrid, Florentino Pérez, amemuweka Olise kama moja ya malengo makuu ya usajili, akiamini kuwa nyota huyo anaweza kuwa mradi mpya wa muda mrefu katika kikosi cha Santiago Bernabéu.
Inadaiwa Pérez anataka kumsajili Olise kama “zawadi ya kwanza” kwa kocha mpya au anayetarajiwa kupewa majukumu makubwa, José Mourinho, huku klabu hiyo ikiwa katika kipindi cha mabadiliko ya kisiasa kuelekea uchaguzi wa klabu unaotarajiwa kufanyika Jumapili, Juni 7, 2026.
Hata hivyo, Bayern Munich wameweka msimamo mkali kwamba nyota huyo hauzwi. Mwenyekiti wa heshima wa klabu hiyo, Uli Hoeness, ameripotiwa kusisitiza kuwa Olise ni sehemu muhimu ya mipango ya muda mrefu ya Bayern na hawana mpango wa kumuuza, badala yake wako tayari kuboresha mkataba wake na mshahara wake ili kumbakiza Allianz Arena.
Olise, ambaye bado ana mkataba hadi mwaka 2029, amekuwa na msimu bora uliojaa ubunifu, mabao na pasi za mwisho, hatua iliyomuweka miongoni mwa wachezaji waliovutia zaidi barani Ulaya. Mafanikio yake yalimfanya kutunukiwa tuzo ya Mchezaji Bora anayecheza nje ya Ufaransa, ishara ya ukuaji wake mkubwa katika soka la kimataifa.
Licha ya msimamo wa Bayern, Real Madrid wanaonekana kutokata tamaa, wakiamini kuwa ofa yao kubwa inaweza kubadilisha maamuzi ya Wajerumani. Mashabiki wa Los Blancos sasa wanasubiri kuona kama Bernabéu itampokea Olise kama mrithi wa kizazi kipya cha mastaa wa klabu hiyo.



