Nahodha mkongwe na mmoja wa wachezaji waliodumu kwa muda mrefu zaidi katika historia ya Ligi Kuu England, James Milner, ametangaza kustaafu soka la kulipwa akiwa na umri wa miaka 40, akihitimisha safari ya kipekee iliyodumu kwa takribani miaka 24 kwenye kiwango cha juu cha soka.
Milner alianza safari yake ya soka la kulipwa akiwa kijana mdogo mwenye umri wa miaka 16 alipocheza kwa mara ya kwanza akiwa na Leeds United mwaka 2002. Tangu hapo, ameandika historia ya kipekee kwa kuchezea vilabu vikubwa tofauti nchini England ikiwemo Newcastle United, Aston Villa, Manchester City, Liverpool na Brighton & Hove Albion.
Katika kipindi chote cha uchezaji wake, Milner ameweka rekodi ya kucheza mechi 658 katika Ligi Kuu England, ikiwa ni idadi kubwa zaidi kuwahi kufikiwa na mchezaji yeyote katika historia ya ligi hiyo. Rekodi hiyo ilimuweka kileleni kama mchezaji mwenye uimara, nidhamu na uthabiti wa kiwango cha juu kwa zaidi ya miongo miwili.
Mbali na rekodi ya mechi, Milner ameondoka akiwa ameshinda mataji makubwa ikiwemo ubingwa wa Ligi Kuu England mara tatu, Kombe la FA, Kombe la Ligi pamoja na taji la UEFA Champions League akiwa na Liverpool. Pia amecheza mechi 61 akiwa na timu ya taifa ya England, akishiriki mashindano makubwa kama Kombe la Dunia na Euro.
Katika taarifa yake ya kustaafu, Milner ameeleza kuwa uamuzi huo umetokana na kuona ni wakati sahihi wa kupumzika baada ya safari ndefu yenye mafanikio makubwa. Ameeleza pia kuwa zaidi ya mataji na rekodi, kilichomgusa zaidi ni mahusiano na watu aliokutana nao katika safari yake ya soka.
Mashabiki na wachambuzi wa soka wamemuelezea Milner kama “mchezaji wa mfano” kutokana na uwezo wake wa kucheza nafasi nyingi uwanjani, nidhamu yake ya hali ya juu na weledi wake wa kipekee ambao ulimsaidia kudumu katika kiwango cha juu kwa muda mrefu.



