Okello atupia mbili Yanga ikiichapa Singida BS 3-0 na kurudi kileleni

Joel JJ By Joel JJ • 22nd May 2026


Okello atupia mbili Yanga ikiichapa Singida BS 3-0 na kurudi kileleni

Yanga imeonyesha ubora wake tena baada ya kuibuka na ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya Singida Black Stars F.C. katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa kwenye uwanja wa KMC Complex.

Nyota wa mchezo alikuwa kiungo mshambuliaji Allan Okello maarufu kama ‘Star Boy’, aliyefunga mabao mawili na kuendelea kuwa nguzo muhimu ndani ya kikosi cha Yanga msimu huu.

Okello alianza kuandika bao la uongozi dakika ya 14 akifunga bao safi la mpira wa adhabu lililomuacha mlinda lango wa Singida BS, Metacha Mnata, akiwa hana la kufanya.

Baada ya bao hilo, benchi la ufundi la Singida BS lilifanya mabadiliko ya haraka kwa kumtoa Metacha na nafasi yake kuchukuliwa na Amos Abasogie. Hata hivyo, mabadiliko hayo hayakuweza kuizuia Yanga kuendelea kutawala mchezo.

Bao la pili la Yanga lilifungwa dakika ya 42 kupitia Mudathir Yahya aliyemalizia mpira uliokuwa umeokolewa awali na mlinda lango wa Singida BS.

Licha ya kuongoza kwa mabao mawili kipindi cha kwanza, Yanga ingeweza kwenda mapumziko ikiwa na ushindi mkubwa zaidi kama Okello, Mudathir pamoja na Maxi Nzengeli wangetumia vizuri nafasi walizozipata.

Kipindi cha pili kilianza kwa Yanga kuendelea kushambulia kwa kasi huku Singida BS wakionekana kushindwa kuhimili presha ya mabingwa hao watetezi. Dakika ya 69, Okello alifunga bao lake la pili na la tatu kwa Yanga, akihitimisha ushindi huo muhimu.

Mabao hayo yamemfikisha Okello kwenye mabao 9 msimu huu, sawa na mshambuliaji Prince Dube ambaye alikuwa akiongoza kwa mabao ndani ya kikosi hicho kabla ya mchezo huo.

Ushindi huo unaifanya Yanga kufikisha alama 57 na kurejea kileleni mwa msimamo wa ligi, wakiwaacha watani zao Simba SC kwenye nafasi ya pili na alama 55.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.