Nahodha wa zamani wa Real Madrid na Spain, Sergio Ramos, ameibuka kwenye headlines za soka Ulaya baada ya taarifa kueleza kuwa yuko kwenye mpango wa kuinunua klabu yake ya zamani ya Sevilla FC kupitia kundi la wawekezaji wa kimataifa.
Vyombo mbalimbali vya habari nchini Hispania vimeripoti kuwa Ramos pamoja na kampuni yake ya uwekezaji wameanza mazungumzo rasmi na baadhi ya wanahisa wakubwa wa Sevilla kuhusu uwezekano wa kubadili umiliki wa klabu hiyo inayopitia kipindi kigumu kifedha na kiushindani.
Kwa mujibu wa ripoti hizo, thamani ya dili hilo inaweza kufikia zaidi ya euro milioni 400 iwapo makubaliano yote yatakamilika katika miezi ijayo.
SEVILLA YAPITIA WAKATI MGUMU
Sevilla imekuwa ikikumbwa na changamoto kubwa katika misimu ya hivi karibuni licha ya historia yake kubwa katika michuano ya UEFA Europa League.
Mbali na kushuka kiwango ndani ya La Liga, klabu hiyo pia imekuwa ikikabiliwa na migogoro ya kiuongozi pamoja na madeni makubwa yaliyoathiri mipango ya maendeleo ya timu.
Wachambuzi wa soka nchini Hispania wanaamini hali hiyo ndiyo iliyowavutia wawekezaji mbalimbali kuonyesha nia ya kuwekeza ndani ya klabu hiyo maarufu ya Andalusia.
RAMOS KUREJEA KLABUNI KWA NAMNA MPYA
Sergio Ramos alianza safari yake ya soka Sevilla kabla ya kuhamia Real Madrid mwaka 2005 ambapo alijijengea jina kubwa duniani kwa kushinda mataji mengi ikiwemo UEFA Champions League na La Liga.
Baada ya kuondoka Madrid, Ramos aliwahi kurejea Sevilla kama mchezaji kabla ya kuanza kufikiria maisha ya nje ya uwanja.
Sasa, taarifa za uwezekano wa kuingia kwenye umiliki wa klabu hiyo zimezua mjadala mkubwa miongoni mwa mashabiki wa soka nchini Hispania.
Baadhi ya mashabiki wanaamini Ramos anaweza kuirudisha Sevilla kwenye mafanikio kutokana na uzoefu wake mkubwa wa soka la kiwango cha juu, huku wengine wakitaka kuona kwanza mipango yake ya muda mrefu kwa klabu hiyo.
MAJADILIANO YAENDELEA
Taarifa kutoka Hispania zinaeleza kuwa mazungumzo kati ya upande wa Ramos na baadhi ya wanahisa wa Sevilla bado yanaendelea huku masuala ya kifedha na kisheria yakipewa uzito mkubwa kabla ya kufikiwa kwa makubaliano rasmi.
Iwapo dili hilo litafanikiwa, Ramos ataingia kwenye orodha ya mastaa wa zamani wa soka waliogeuka kuwa wawekezaji au wamiliki wa vilabu baada ya kustaafu kucheza.
Mashabiki wa Sevilla kwa sasa wanaendelea kufuatilia kwa karibu maendeleo ya mazungumzo hayo huku wengi wakiamini kuwa mabadiliko ya uongozi yanaweza kuwa mwanzo mpya kwa klabu hiyo.
Hadi sasa Sevilla haijatoa taarifa rasmi kuhusu mazungumzo hayo, lakini jhuenda mpango huo ukakamilishwa.



