Barker apania kuvuna alama 30 mechi 10 zilizobaki

Joel JJ By Joel JJ • 5th May 2026


Barker apania kuvuna alama 30 mechi 10 zilizobaki

Kocha Mkuu wa Simba SC, Steve Barke, amesema timu yake bado haijakata tamaa katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu NBC licha ya kuwa nyuma kwa tofauti ya alama tano dhidi ya vinara, Yanga.

Akizungumza kuelekea michezo iliyosalia, Barker ameweka wazi kuwa bado kuna alama 30 za kuwania katika mechi 10 zilizosalia, akisisitiza kuwa lengo lao ni kuhakikisha wanashinda kila mchezo uliopo mbele yao.

“Bado tuna nafasi, kuna alama 30 za kupigania hivyo jambo muhimu kwetu ni kuhakikisha tunafanya vyema kwenye kila mchezo,” alisema Barker.

Kocha huyo ameongeza kuwa benchi la ufundi linaangazia kila mechi mmoja baada ya mwingine, wakianzia na mchezo wao ujao dhidi ya JKT Tanzania.

“Tutaweka malengo yetu kwenye kila mechi, hivyo kwa sasa tunatazama mchezo ulio mbele yetu dhidi ya JKT Tanzania.”

Barker ameonya kuwa mchezo huo hautakuwa mwepesi, akieleza kuwa JKT Tanzania ni timu yenye ushindani mkubwa, kocha mwenye mbinu na wachezaji wanaopambana kwa nguvu uwanjani.

“Ni mechi ngumu dhidi ya JKT Tanzania, kwani ni timu yenye kocha mzuri na wachezaji wenye moyo wa kupambana.”

Amesisitiza umuhimu wa nidhamu ya mbinu na utekelezaji sahihi wa mipango ya mchezo ili kufanikisha malengo yao ya kukusanya alama zote zinazowezekana.

“Tunapaswa kuweka mkazo katika mbinu na mipango yetu ili kuhakikisha tunaendelea kucheza vizuri na kufanya vyema kwenye kila mchezo tukianza na huo wa kesho.”

Mchezo kati ya Simba SC na JKT Tanzania unatarajiwa kupigwa kesho Jumatano saa 12:15 jioni, ukiwa ni siku tatu tangu Simba ipate sare ya mabao 2-2 dhidi ya Young Africans SC katika dabi ya Kariakoo iliyochezwa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo.

Kwa sasa, presha inaendelea kuongezeka katika mbio za ubingwa, huku Simba wakihitaji ushindi mfululizo ili kuendelea kuweka hai matumaini yao ya kutwaa taji msimu huu.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.