Nani ataizuia Yanga? mechi 40 bila kupoteza ligi kuu

Joel JJ By Joel JJ • 4th May 2026


Nani ataizuia Yanga? mechi 40 bila kupoteza ligi kuu

Yanga wameendelea kuandika historia katika Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kufikisha mechi 40 bila kupoteza, kufuatia sare ya mabao 2-2 dhidi ya Simba SC katika mchezo uliopigwa jana.

Matokeo hayo yanaendeleza rekodi ndefu ya kutopoteza kwa Yanga, ambao wamekuwa wakionekana kuwa moja ya vikosi imara zaidi katika soka la Tanzania kwa kipindi cha miaka ya hivi karibuni.

Kwa mujibu wa takwimu za ligi, mara ya mwisho Yanga kupoteza mchezo wa Ligi Kuu ilikuwa Novemba 7, 2024, walipofungwa mabao 3-1 na Tabora United, ambao kwa sasa wanajulikana kama TRA United.

Tangu wakati huo, Yanga wamekuwa na mwendelezo mzuri wa matokeo, hali iliyowasaidia kufikia hatua ya sasa ya mechi 40 bila kupoteza.

Takwimu zinaonesha kuwa klabu hiyo sasa imebakiza mechi tisa kufikia rekodi yao ya awali ya mechi 49 bila kupoteza, ambayo waliiweka misimu miwili iliyopita. Endapo watamaliza msimu bila kupoteza katika mechi zao zilizobaki, watafanikiwa kuvunja rekodi yao wenyewe na kuweka kiwango kipya katika historia ya ligi.

Katika historia ya Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga ndiyo klabu inayoshikilia rekodi bora zaidi za kutopoteza, ikiwa imeweka rekodi mbili kubwa za mechi 49 na 40 bila kupoteza, huku Simba SC na Azam FC zikifuata kwa rekodi za karibu za mechi 37 bila kupoteza.

Wachambuzi wa soka wanasema mafanikio haya yanaonyesha uthabiti wa kiufundi, nidhamu ya wachezaji na uongozi imara ndani ya kikosi cha Yanga.

Huku msimu ukiendelea, swali ni je Yanga wataweza kuvuka rekodi yao wenyewe na kuandika ukurasa mpya?.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.