Mshambuliaji wa kimataifa wa Kenya, Elvis Rupia, ameondoka katika klabu ya Singida Black Stars (Singida BS) aliyokuwa akiitumikia, kufuatia mgogoro unaodaiwa kuhusiana na malipo ya fedha za usajili.
Kwa mujibu wa chanzo cha karibu na mchezaji huyo, Rupia amekuwa na mvutano na uongozi wa klabu hiyo kutokana na madai ya kutolipwa stahiki zake, hali iliyopelekea kufikia uamuzi wa kuondoka.
Inaelezwa kuwa hadi sasa hakuna mwafaka uliopatikana kati ya pande hizo mbili, jambo linalotia shaka uwezekano wa mshambuliaji huyo kurejea kikosini kabla ya msimu huu kumalizika.
Rupia, ambaye ni miongoni mwa washambuliaji wenye uzoefu katika ukanda wa Afrika Mashariki, ameichezea Singida BS kwa kipindi cha misimu mitatu, akitoa mchango wake katika safu ya ushambuliaji ya timu hiyo.



