Simba yafuata mbadala wa Sowah Chad

Joel JJ By Joel JJ β€’ 28th April 2026


Simba yafuata mbadala wa Sowah Chad

Simba SC imeanza mapema harakati za kujijenga upya kuelekea msimu ujao, huku ikitajwa kuelekeza nguvu zake katika kusaka mshambuliaji mpya wa kuimarisha safu ya ushambuliaji.

Taarifa za hivi karibuni zinaeleza kuwa Wekundu wa Msimbazi wanamfuatilia kwa karibu mshambuliaji raia wa Chad, Junior Dion, anayekipiga katika klabu ya Golden Arrows ya Afrika Kusini.

Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 27 anaripotiwa kuvutia macho ya mabosi wa Simba baada ya kuwa na msimu mzuri, ambapo alifanikiwa kufunga mabao 14 pamoja na kutoa pasi za mabao katika mashindano mbalimbali.

Uwezo wake wa kufumania nyavu na kushiriki katika ujenzi wa mashambulizi umeonekana kuwa suluhisho kwa Simba, ambayo imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya kupata mabao ya kutosha kutoka kwa washambuliaji wake wa kati.

Simba yatafuta mbadala wa Sowah

Hatua ya Simba kuingia sokoni inakuja kufuatia sintofahamu iliyopo kati ya klabu hiyo na mshambuliaji wake, Jonathan Sowah.

Mchezaji huyo aliwahi kusimamishwa na klabu kutokana na tuhuma za utovu wa nidhamu, na baada ya kesi yake kusikilizwa, alitakiwa kulipa faini pamoja na kushushwa kucheza na kikosi cha vijana (U20) ili kurejesha utimamu wake.

Hata hivyo, taarifa zinaeleza kuwa Sowah hajatekeleza maamuzi hayo kikamilifu, huku akidai kuvunja mkataba wake kwa makubaliano ya pande zote mbili β€” jambo linalozidi kuongeza sintofahamu ndani ya klabu.

Mkakati mpya wa Simba

Kutokana na hali hiyo, Simba inaonekana kuanza safari ya kusaka mrithi wa uhakika katika nafasi ya ushambuliaji, huku jina la Junior Dion likitajwa kuwa miongoni mwa wachezaji wanaopewa kipaumbele.

Iwapo dili hilo litafanikiwa, basi Dion anaweza kuwa sehemu muhimu ya kikosi cha Simba kitakacholenga kufanya vizuri katika mashindano ya ndani na yale ya kimataifa msimu ujao.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.