Hatimaye pazia la nusu fainali limefungwa kwa kishindo, na sasa macho yote yanaelekezwa kwenye dabi ya Kariakoo baada ya Simba SC kutinga fainali ya Kombe la Muungano kwa ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya Mlandege FC.
Mchezo huo uliopigwa katika dimba la New Amaan Complex ulishuhudia Simba ikionyesha ubora mkubwa licha ya kocha Steve Barker kufanya mabadiliko makubwa ya kikosi na kuwaacha nje baadhi ya nyota wake wa kikosi cha kwanza.
Tangu dakika za mwanzo, Wekundu wa Msimbazi walitawala mchezo huo wakitengeneza nafasi kadhaa za mabao, huku Elie Mpanzu aliyekuwa akicheza nafasi ya mshambuliaji kivuli akikosa nafasi kadhaa ambazo zingeiwezesha timu yake kwenda mapumziko ikiwa mbele.
Kipindi cha pili kilileta sura mpya kabisa baada ya Barker kufanya mabadiliko muhimu kwa kuwaingiza Yusuph Kagoma, Suleiman Mwalimu, Anicet Oura pamoja na Clatous Chama β mabadiliko yaliyobadilisha mwelekeo wa mchezo.
Ilichukua hadi dakika ya 63 kwa Simba kupata bao la kwanza kupitia kwa Suleiman Mwalimu aliyemalizia pasi safi kutoka kwa Clatous Chama, aliyefanya kazi kubwa pembezoni mwa uwanja.
Dakika ya 76, Anicet Oura akaongeza bao la pili kwa pasi nyingine ya Chama, huku kiungo huyo akitawala dimba la kati akishirikiana vyema na Kagoma pamoja na Neo Maema.
Bao la tatu lilifungwa na Maema katika dakika za lala salama kwa shuti kali nje kidogo ya eneo la hatari, akihitimisha ushindi huo wa kishindo.
Maema aliibuka kuwa nyota wa mchezo baada ya kiwango bora alichoonyesha kwa dakika zote 90, akiongoza safu ya kiungo kwa ubunifu na nidhamu ya hali ya juu.
Ushindi huo unaifanya Simba sasa kukutana na watani wao wa jadi, Young Africans SC, katika fainali ya Kombe la Muungano itakayopigwa Aprili 29.
Hii inaweka wazi ratiba ya moto kwa mashabiki wa soka nchini, kwani ndani ya kipindi cha wiki moja kutashuhudiwa dabi mbili za Kariakoo, ya kwanza ikiwa ni fainali ya Muungano Cup, kabla ya miamba hiyo kukutana tena Mei 3 kwenye mchezo wa Ligi Kuu utakaopigwa katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo Stadium.



