Kiungo nahodha wa Manchester United, Bruno Fernandes, amepewa uhakika wa mustakabali wake klabuni hapo kufuatia taarifa mpya zinazoonyesha kuwa hataruhusiwa kuondoka katika dirisha lijalo la usajili.
Kwa mujibu wa taarifa za hivi karibuni, uongozi wa Manchester United umeweka wazi kuwa hauna mpango wowote wa kumuachia nyota huyo, ukisisitiza kuwa hatouzwa “kwa hali yoyote” katika majira ya joto yajayo.
Hatua hiyo inakuja baada ya kipindi cha sintofahamu kilichohusisha ofa kubwa kutoka klabu za Saudi Arabia, ikiwemo ofa ya Al-Nassr iliyodaiwa kufikia pauni milioni 80. Hata hivyo, mabosi wa United sasa wamebadilisha msimamo na kumhakikishia nahodha wao kuwa ni sehemu muhimu ya mipango ya muda mrefu ya klabu.
Ripoti nyingine zinaeleza kuwa klabu pia imeanza juhudi za kuharakisha mazungumzo ya kuongeza mkataba mpya ili kumfunga zaidi kiungo huyo, ambaye tayari ana mkataba unaoelekea kumalizika ndani ya kipindi kifupi kijacho.
Mbali na msimamo huo wa klabu, Fernandes mwenyewe ameonyesha dalili za kuridhika kuendelea kubaki Old Trafford, akisisitiza furaha yake na nafasi yake ndani ya timu hiyo.
Kwa sasa, nyota huyo anaendelea kuwa mhimili muhimu wa kikosi cha United, akichangia mabao na pasi za mwisho huku akiongoza timu kama nahodha. Uongozi wa klabu unaamini kuwa mafanikio ya msimu huu, ikiwa ni pamoja na mbio za kufuzu michuano ya Ulaya, yatasaidia zaidi kumshawishi kubaki.



