Simba yaendeleza ubabe ligi kuu, yaichapa Namungo 3-1

Joel JJ By Joel JJ β€’ 19th April 2026


Simba yaendeleza ubabe ligi kuu, yaichapa Namungo 3-1

Klabu ya Simba SC imeendelea kuonesha ubora wake katika NBC Premier League baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Namungo FC kwenye dimba la Majaliwa, Ruangwa.

Ilikuwa ni mechi iliyotawaliwa kwa kiasi kikubwa na Wekundu wa Msimbazi, wakionesha dhamira ya wazi ya kusaka alama tatu muhimu. Simba ilianza kwa kasi ambapo dakika ya 12, mshambuliaji Libasse Gueye alifungua ukurasa wa mabao baada ya kupokea pasi murua kutoka kwa Anthony Mligo ndani ya eneo la hatari.

Mashambulizi ya Simba yaliendelea kuisumbua safu ya ulinzi ya Namungo, na dakika ya 25, kiungo Anicet Oura aliongeza bao la pili kwa shuti kali nje kidogo ya eneo la mita 18 lililomshinda mlinda lango wa wenyeji.

Namungo walijaribu kurejea mchezoni na dakika ya 33 wakapata mkwaju wa penati uliozua mjadala, baada ya mwamuzi kudai kuwa mpira ulimgonga beki Yusuph Kagoma licha ya kuonekana kama alikuwa ameficha mikono yake. Heritier Makambo aliifungia Namungo penati hiyo na kupunguza pengo.

Kipindi cha pili kilianza kwa Namungo kujaribu kusaka bao la kusawazisha, lakini juhudi zao hazikuzaa matunda. Badala yake, ilikuwa ni Simba waliothibitisha ubora wao zaidi pale Elie Mpanzu alipofunga bao la tatu dakika ya 74, akihitimisha ushindi huo muhimu.

Matokeo hayo yanaifanya Simba kufikisha alama 42 na kuendelea kushikilia nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi. Wekundu hao sasa wamepunguza pengo la pointi dhidi ya watani wao Yanga hadi kufikia alama tano pekee.

Macho sasa yanaelekezwa kwenye pambano kubwa lijalo, Derby ya Kariakoo itakayopigwa Mei 03, mechi inayotarajiwa kuwa na ushindani mkali na kuamua mwelekeo wa mbio za ubingwa.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.