Real Sociedad yaiduwaza Atletico Madrid, yatwaa Copa Del Rey

Joel JJ By Joel JJ • 19th April 2026


Real Sociedad yaiduwaza Atletico Madrid, yatwaa Copa Del Rey

Klabu ya Atletico Madrid imekosa nafasi ya kutwaa ubingwa wa Copa del Rey 2026 kufuatia kupoteza kwa mikwaju ya penalti dhidi ya Real Sociedad katika fainali iliyochezwa Aprili 18, 2026 jijini Sevilla.

Mchezo huo ulikuwa wa kusisimua kuanzia mwanzo hadi mwisho, ukimalizika kwa sare ya mabao 2-2 ndani ya dakika 120 kabla ya kuamuliwa kwa penalti. Real Sociedad waliibuka washindi kwa ushindi wa penalti 4-3, wakitwaa taji hilo kwa mara ya nne katika historia yao.

Atletico walijikuta wakianza vibaya baada ya kuruhusu bao la mapema kabisa, lakini walijibu kupitia kwa Ademola Lookman kabla ya Real Sociedad kurejesha uongozi kupitia penalti ya Mikel Oyarzabal. Kipindi cha pili kilishuhudia juhudi za Atletico zikizaa matunda baada ya Julián Álvarez kusawazisha dakika za mwisho na kulazimisha muda wa ziada.

Hata hivyo, katika hatua ya mikwaju ya penalti, mlinda mlango wa Real Sociedad, Unai Marrero, aliibuka shujaa baada ya kuokoa penalti mbili muhimu na kuihakikishia timu yake ushindi huo wa kihistoria.

Kocha wa Atletico, Diego Simeone, alionesha masikitiko makubwa baada ya mchezo huo, akisisitiza kuwa timu yake ilipata nafasi za kushinda ndani ya dakika 90 lakini ilishindwa kuzitumia ipasavyo.

Matokeo hayo yanaiacha Atletico Madrid ikiendelea kusubiri taji la ndani, huku matumaini yao yakibaki katika mashindano mengine kama Ligi ya Mabingwa Ulaya. Kwa upande wa Real Sociedad, ushindi huo unaashiria mafanikio makubwa na kurudi kileleni mwa soka la Hispania.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.