Klabu ya Bayern Munich imefanikiwa kutinga hatua ya nusu fainali ya UEFA Champions League baada ya kuibuka na ushindi wa kusisimua wa mabao 4-3 dhidi ya Real Madrid, na kufuzu kwa jumla ya mabao 6-4.
Mchezo huo uliochezwa katika dimba la Allianz Arena ulikuwa na kila kitu, mabao ya mapema, mabadiliko ya matokeo na tamati ya kushtua, ambapo Real Madrid walianza kwa kasi kupitia Arda Güler aliyefunga bao la mapema kabisa dakika ya kwanza, kabla ya Bayern kujibu kupitia Aleksandar Pavlovi dakika ya 6. Hata hivyo, Arda Güler alifanikiwa kuongeza bao lingine dakika ya 29 kupitia freekick na kuiweka timu yake mbele. Na baadae Harry Kane alifunga dakika ya 38, kabla ya Kylian Mbappé kuifungia tena Real Madrid bao la tatu dakika ya 42 na kuisaidia timu yake kuongoza.
Dakika za mwisho ndizo zilizoamua hatima ya mchezo. Luis Díaz aliisawazishia Bayern dakika ya 89, kabla ya Michael Olise kufunga bao la ushindi dakika ya 90+4, bao lililozima kabisa matumaini ya Real Madrid.
Ushindi huo unaifanya Bayern kufika nusu fainali ya mashindano hayo kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2020, wakionyesha kurejea kwa nguvu katika ushindani wa soka la Ulaya.
Kwa upande wa Real Madrid, kuondolewa huku kunaongeza presha kubwa ndani ya klabu hiyo, huku wakikabiliwa na hatari ya kumaliza msimu bila taji, hasa wakizingatia hali yao katika La Liga ambapo wanashindana kwa karibu na vinara wa ligi hiyo Barcelona.



