Kamwe afunguka maandalizi ya Yanga kuikabili Mbeya City

Joel JJ By Joel JJ • 14th April 2026


Kamwe afunguka maandalizi ya Yanga kuikabili Mbeya City

Maandalizi ya kikosi cha Young Africans SC kuelekea mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mbeya City FC yanaendelea kwa umakini mkubwa, huku klabu hiyo ikisisitiza dhamira ya kuendeleza ubora wake katika mbio za ubingwa.

Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga, Ali Kamwe, amesema maandalizi ya mchezo huo unaotarajiwa kupigwa Alhamisi Aprili 16 katika Uwanja wa KMC Complex yako katika hatua nzuri, lakini yakifanyika kwa tahadhari kubwa kutokana na ushindani wa ligi msimu huu.

Kamwe amesema Yanga inatambua kuwa mchezo dhidi ya Mbeya City hautakuwa mwepesi, hasa ukizingatia historia ya matokeo ya duru ya kwanza ambapo timu hizo zilitoshana nguvu kwa suluhu ya bila kufungana katika Uwanja wa Sokoine Stadium

“Hatukuondoka na pointi tatu kwenye mchezo wa kwanza, sasa tunarudi KMC Complex tukiwa nyumbani. Dhamira yetu ni kuona tunafanya vizuri zaidi,” alisema Kamwe.

Ameongeza kuwa mkakati wa Yanga kwa sasa hauishii tu katika kutafuta ushindi wa mchezo mmoja mmoja, bali ni kuhakikisha timu inakuwa na mwendelezo wa matokeo bora ili kutetea ubingwa wake.

“Sasa tuko raundi ya pili, ligi imeshachanganya. Dhamira yetu imebadilika, siyo kumfunga Mbeya City tu, bali kuwa na mwendelezo mzuri ili kuhakikisha tunatetea ubingwa wetu kwa mara ya tano mfululizo,” alifafanua.

Kamwe amesema hali hiyo imewapa motisha wachezaji na benchi la ufundi, huku akibainisha kuwa maandalizi yameanza rasmi baada ya kikosi kurejea mazoezini jana.

“Ni dhamira hiyo ambayo itatufanya sisi Yanga tuende kwenye mchezo huo tukiwa na ari kubwa. Tutacheza kwa kujituma na kujitolea ili kuhakikisha tunashinda na kuendelea kujiweka katika nafasi nzuri kwenye mbio za ubingwa,” alisema.

Kamwe amethibitisha kurejea kikosini kwa wachezaji Djigui Diarra, Prince Dube na Depu ambaye hata hivyo amesema bado hayuko fit kwa asilimia 100.

Diarra amemaliza adhabu ya kufungiwa mechi tatu huku Dube na Depu wakirejea baada ya kupona majeraha.

Aidha msemaji huyo wa mabingwa watetezi ligi kuu ya NBC, amesema mshambuliaji Emmanuel Mwanengo bado ni majeruhi kama ilivyo kwa Buba Jammeh aliyeumia katika mchezo wa kombe la CRDB dhidi ya TMA Stars.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.