Tanzania yapoteza Fainali ya AFCON U-17 kwa Penalti

Joel JJ By Joel JJ β€’ 3rd June 2026


Tanzania yapoteza Fainali ya AFCON U-17 kwa Penalti

Safari ya kihistoria ya Serengeti Boys katika Kombe la Mataifa ya Afrika kwa vijana chini ya miaka 17 (AFCON U-17) imefikia tamati kwa uchungu baada ya Tanzania kupoteza kwa mikwaju ya penalti 4-2 dhidi ya Senegal kufuatia sare ya mabao 1-1 katika fainali iliyochezwa usiku wa Jumanne mjini Rabat, Morocco.

Licha ya kutwaa nafasi ya pili, Tanzania imeandika historia kwa kufika fainali ya mashindano hayo kwa mara ya kwanza kabisa huku ikithibitisha ukuaji mkubwa wa soka la vijana nchini.

Serengeti Boys walianza mchezo kwa kasi na kufanikiwa kupata bao la mapema dakika ya saba kupitia Hamis Chenga, aliyemalizia vyema shambulizi lililoishtua safu ya ulinzi ya Senegal. Bao hilo liliwapa matumaini makubwa mashabiki wa Tanzania waliokuwa wakifuatilia mchezo huo kwa hamasa kubwa.

Baada ya kuruhusu bao hilo, Senegal waliinua kiwango chao cha mchezo na kuanza kushambulia kwa nguvu wakisaka bao la kusawazisha huku Tanzania ikijikita zaidi katika kulinda uongozi wake.

Kipindi cha pili kilianza kwa presha kubwa kutoka kwa vijana wa Senegal ambao walitawala sehemu kubwa ya mchezo. Juhudi zao zilizaa matunda dakika ya 64 pale Ibrahima Dione alipotikisa nyavu baada ya kipa wa Tanzania kuokoa mpira wa adhabu uliopigwa na Souleymane Commissaire Faye na kuacha mpira ukimwangukia mshambuliaji huyo.

Timu zote zilipata nafasi kadhaa za kufunga katika dakika zilizobaki lakini hakuna iliyoweza kupata bao la ushindi ndani ya dakika 90 za kawaida, hali iliyosababisha bingwa kuamuliwa kwa mikwaju ya penalti.

Katika hatua ya mikwaju ya penalti, Senegal walionyesha utulivu mkubwa kwa kufunga penalti zao zote nne. Tanzania ilishindwa kuhimili presha baada ya Kilendemo na Mbegu kukosa mikwaju yao, jambo lililoipa Senegal ushindi wa penalti 4-2 na kutwaa ubingwa wa Afrika.

Matokeo hayo yaliifanya Senegal kutwaa taji la AFCON U-17 huku Tanzania ikibaki na medali za fedha baada ya kampeni iliyovutia wengi barani Afrika.

Tanzania yaondoka na tuzo kadhaa

Pamoja na kupoteza fainali, Tanzania imeondoka Morocco ikiwa na mafanikio makubwa. Serengeti Boys walitwaa tuzo ya Fair Play, huku Dismas Athanasi Elieneza akimaliza mashindano akiwa mfungaji bora kwa mabao matatu. Aidha, Issa Chole alichaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Mashindano.

Kocha Elieneza Nsanganzelu alisema timu yake ina sababu nyingi za kujivunia licha ya kushindwa kutwaa ubingwa.

"Ni mafanikio makubwa kufuzu Kombe la Dunia la FIFA U-17 na kufika fainali ya AFCON kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania," alinukuliwa akisema baada ya mchezo.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.