Kocha Msaidizi wa Simba SC, Suleiman Matola, amesema mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Dodoma Jiji FC utakaopigwa kesho Jumapili katika uwanja wa KMC Complex hautakuwa mwepesi, akisisitiza kuwa wapinzani wao ni timu yenye ubora na ushindani mkubwa.
Akizungumza na wanahabari kuelekea mchezo huo, Matola amesema wanakumbuka ugumu walioupata mara ya mwisho walipokutana na Dodoma Jiji mkoani Dodoma, ambapo mchezo huo uliishia kwa suluhu ya bila kufungana.
Hata hivyo, amesisitiza kuwa Simba imejipanga vyema kuhakikisha inapata alama zote tatu muhimu zitakazowasaidia kurejea kileleni mwa msimamo wa ligi.
“Haitakuwa mechi rahisi ukiangalia matokeo ya mchezo uliopita, Dodoma Jiji walitupa wakati mgumu,” alisema Matola.
“Lakini pamoja na ugumu na ubora wao, tumejipanga kuhakikisha tunapata pointi tatu katika mchezo huo.”
Wakati huo huo, kikosi cha Simba kilirejea jijini Dar es Salaam jana kikitokea mkoani Tanga, ambako kiliibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Coastal Union, matokeo ambayo yameongeza morali ndani ya kikosi hicho kabla ya mchezo huu muhimu wa ligi.



