Simba bado imo 10 bora CAF, Yanga haiko mbali

Joel JJ By Joel JJ β€’ 20th April 2026


Simba bado imo 10 bora CAF, Yanga haiko mbali

Klabu ya Simba SC imeendelea kusalia miongoni mwa klabu 10 bora katika viwango vya Shirikisho la Soka Afrika (CAF), licha ya msimu wake wa changamoto kwenye michuano ya CAF Champions League.

Simba ilimaliza hatua ya makundi ikiwa nafasi ya nne Kundi D, matokeo ambayo yaliwakatisha tamaa baadhi ya mashabiki waliotarajia mafanikio makubwa zaidi msimu huu. Hata hivyo, wengi walidhani klabu hiyo ingeporomoka zaidi kwenye viwango vya CAF kutokana na matokeo hayo.

Lakini tofauti na matarajio, Simba imeendelea kushikilia nafasi ndani ya klabu 10 bora Afrika, ikionesha uimara wake wa muda mrefu katika michuano ya kimataifa.

Kwa mujibu wa viwango vipya vya CAF vilivyotolewa baada ya kukamilika kwa hatua za nusu fainali za Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho, Simba imeshika nafasi ya 10 barani Afrika, ikiwa na alama 38.

Simba imefungana kwa alama na klabu ya CR Belouizdad ambayo msimu huu imefanikiwa kufika nusu fainali ya kombe la Shirikisho (CAFCC) .

Kwenye nafasi za juu, klabu ya Mamelodi Sundowns imepanda hadi kileleni mwa orodha baada ya kufanya vizuri kwenye mashindano ya CAF msimu huu.

Al Ahly SC nayo imeendelea kuwa miongoni mwa vigogo, ingawa imeshuka kidogo hadi nafasi ya pili kutokana na ushindani mkubwa kutoka kwa Sundowns.

Katika upande mwingine, klabu ya USM Alger pamoja na AS FAR Rabat zimepanda viwango baada ya kufanya vizuri kwenye michuano ya CAF msimu huu, zikiingia kwenye orodha ya timu 10 bora.

Pia Al Hilal Club imefanikiwa kujiimarisha ndani ya orodha hiyo kutokana na matokeo mazuri ya kimataifa.

Klabu ya Yanga imeshika nafasi ya 12 ikiwa na alama 35 Wananchi sasa wakiwa nyuma ya watani zao Simba kwa tofauti ya alama 3 tu wakati Azam Fc na Singida BS zikifungana katika nafasi ya 38 zikiwa na alama 5


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.