Sakata jipya limeibuka kati ya Manchester City na kambi ya uchaguzi wa urais wa Real Madrid baada ya mgombea Enrique Riquelme kudai kuwa amefanikisha mpango wa kumpeleka Erling Haaland Santiago Bernabéu iwapo atashinda uchaguzi wa klabu hiyo.
Riquelme, ambaye anampinga rais wa sasa wa Real Madrid, alizua mjadala mkubwa alipokuwa kwenye kipindi maarufu cha televisheni nchini Hispania akiahidi kuwasajili Haaland pamoja na Rodri kama sehemu ya ahadi zake za uchaguzi.
Mgombea huyo alienda mbali zaidi kwa kuonyesha jezi ya Real Madrid yenye jina la Erling Haaland na kudai kuwa mshambuliaji huyo ana kifungu maalum kinachowezesha kuondoka Manchester City na kwamba anatamani kujiunga na mabingwa hao wa Hispania.
Hata hivyo, madai hayo yalikanushwa haraka na watu wa karibu wa Haaland. Baba yake, Alfie Haaland, pamoja na wakala wake, Rafaela Pimenta, walitoa tamko wakisema kuwa taarifa hizo "zinavutia kusikia lakini si za kweli."
Baada ya kauli hiyo, Manchester City nao walitoa msimamo mkali zaidi. Klabu hiyo imesisitiza kuwa hakuna uwezekano wa Haaland kuhamia Real Madrid kwa sasa na kwamba hakuna kifungu chochote katika mkataba wake kinachoruhusu jambo hilo kutokea.
Zaidi ya hapo, City wameeleza kuwa wanatafakari kuchukua hatua za kisheria kutokana na matumizi ya picha na jina la mchezaji wao katika muktadha wa kampeni za uchaguzi wa Real Madrid.
Taarifa ya Manchester City ilisema:
"Taarifa zilizoibuka kutoka Hispania kuhusu mustakabali wa Erling Haaland si za kweli. Hakuna nafasi ya jambo hilo kutokea na hakuna kifungu cha mkataba kinachoruhusu hilo. Tunafikiria kuchukua hatua za kisheria kuhusu matumizi ya picha ya mchezaji wetu katika muktadha huu."
Chanzo cha mvutano huu ni kampeni za uchaguzi wa urais wa Real Madrid zinazotarajiwa kufanyika mwishoni mwa wiki hii. Riquelme amekuwa akitumia ahadi kubwa za usajili kama njia ya kuvutia kura dhidi ya rais wa muda mrefu wa klabu hiyo, Florentino Pérez.



