Kocha Mkuu wa Yanga SC, Pedro Gonçalves, amewatoa hofu mashabiki wa klabu hiyo kufuatia matokeo ya fainali ya Kombe la Muungano, akisisitiza kuwa kikosi chake sasa kinahamishia nguvu zote kwenye mchezo ujao kwenye ligi dhidi ya watani zao Simba SC.
Yanga ilikubali kichapo cha bao 1-0 katika fainali hiyo iliyochezwa kwenye New Amaan Complex, mchezo uliodumu kwa dakika 120 baada ya dakika 90 kumalizika kwa suluhu ya bila kufungana. Bao pekee la Simba lilipatikana katika muda wa nyongeza kupitia mkwaju wa penati, na kuamua hatima ya taji hilo.
Licha ya maumivu ya kupoteza fainali, Goncalves amewataka mashabiki kuwa watulivu na kuendelea kuiunga mkono timu, akisisitiza mshikamano na umoja ndani ya kikosi.
Katika ujumbe wake, kocha huyo amesema:
“Ninajivunia timu yangu kwa namna tulivyopambana katika Kombe la Muungano. Tumeonesha kujitoa, tabia njema na umoja hadi dakika ya mwisho.”
Ameendelea kuwashukuru mashabiki wa Yanga, maarufu kama Wananchi, kwa sapoti yao kubwa:
“Asanteni Wananchi kwa sapoti yenu ya ajabu, tunaihisi kila hatua ya safari yetu.”
Kocha huyo raia wa Ureno amesema kikosi chake kinarudi uwanjani kuanza maandalizi ya mchezo mwingine mkubwa wa Dabi ya Kariakoo dhidi ya Simba, utakaopigwa Jumapili Mei 03 katika uwanja wa Isamuhyo Mbweni Ground, Dar es Salaam.
Amesema Yanga wanahitaji kuhamisha nguvu zote kuelekea mchezo huo muhimu wa ligi, huku wakiwa bado wanaongoza msimamo:
“Sasa tunahamishia nguvu zote kwenye mchezo wa Jumapili. Tuko kileleni kwa juhudi zetu wenyewe na lazima tuendelee kupigania nafasi hiyo.”
Aidha, amesisitiza umuhimu wa mashabiki kuendelea kuwa sehemu ya timu:
“Tunahitaji muendelee kuwa nasi, sapoti yenu ni muhimu sana. Tunaendelea kufanya kazi, tunaendelea kusukuma mbele — pamoja.”



