Kocha mkuu wa Yanga, Rui Pedro Gonçalves, ameweka wazi kuwa kikosi chake kiko tayari kikamilifu kwa fainali ya Kombe la Muungano dhidi ya Simba SC, huku akisisitiza kuwa mchezo huo hautakuwa wa ushindani pekee bali pia burudani kwa mashabiki.
Mchezo huo mkubwa unatarajiwa kupigwa kesho Jumatano, Aprili 29 katika Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar, ukiwakutanisha wapinzani wakubwa wa soka la Tanzania.
Malengo ni kushinda kila mchezo
Akizungumza na wanahabari kabla ya fainali hiyo, Goncalves amesema Yanga imejipanga kushinda kila mchezo bila kujali ukubwa wa mashindano, huku akisisitiza kuwa nidhamu na malengo ya klabu ndiyo msingi wa mafanikio yao.
“Tulipoanza msimu tuliweka malengo yetu. Ukiachilia mbali mashindano yaliyopewa kipaumbele, msimamo wetu ni kushinda kila mechi,” alisema Goncalves.
Kocha huyo ameongeza kuwa kazi yake kubwa ni kuhakikisha wachezaji wanabaki katika kiwango bora na kuendelea kujiamini katika kila mchezo wanaocheza.
Burudani kwa mashabiki
Goncalves amesisitiza kuwa Yanga haitakwenda uwanjani kwa ajili ya ushindi pekee, bali pia kutoa burudani kwa mashabiki watakaojitokeza kwa wingi kushuhudia fainali hiyo.
“Wachezaji wangu wamejiandaa sio tu kucheza fainali, bali kutoa burudani. Tutakwenda kuburudisha mashabiki na sio tu kucheza,” alifafanua.
Ameongeza kuwa ana matarajio makubwa kutoka kwa kikosi chake, akiamini kuwa mchezo huo utakuwa wa kuvutia na wenye ushindani wa hali ya juu.
Zanzibar ni nyumbani kwa Yanga
Kocha huyo pia aligusia mapokezi mazuri ambayo timu yake imekuwa ikipata kila wanaposafiri sehemu mbalimbali nchini, akisisitiza kuwa Yanga inahisi kama ipo nyumbani popote Tanzania.
“Yanga inapokuwa ndani ya Tanzania Bara au visiwani ipo nyumbani. Tumepata mapokezi mazuri kila sehemu. Hapa Zanzibar tupo nyumbani,” alisema.



